EKARISTI TAKATIFU

   Ekaristi Takatifu ni Sakramenti ya Mwili na damu ya Yesu Kristo, ulio kweli katika Maumbo ya mkate na Divai. Ni fumbo la ukombozi wetu aliloweka kristo siku ya Alhamisi Kuu katika karamu ya mwisho alipoketi kuumega mkate pamoja na wanafunzi wake. Ambapo fumbo hili liliweza kukamilika baada ya Kristo kujitoa sadaka msalabani kwa ajili ya dhambi zetu.

 

   Je, Fumbo Hili la Ekaristi Takatifu, hukamilika wakati gani?

Kama vile Kristo alivoweza kuanzisha Sakramenti hii kwa kuumega mkate na kuikamilisha  katika mlima kalvari (Golgotha), nasi tunaaswa katika ulimwengu wa sasa, kwamba baada ya kuupokea Mwili na damu ya bwana wetu Yesu kristo kupitia maadhimisho ya Misa Takatifu, tunampokea Kristo ndani ya mioyo yetu na kupitia Neema za sakramenti hii, Kristo anaishi ndani yetu nasi ndani yake. Hivo, tunaaswa kwenda kuuishi ukristo wetu katika mazingira na maisha yetu ya kila siku, ili huyu Kristo tuliyekubali kumpokea aishi ndani yetu na ajidhihirishe kupitia matendo yetu mema yanayomtukuza Mwenyezi Mungu, kama vile kuwagusa wahitaji na kuuishi upendo kwa ndugu zetu.

 

   Je, fumbo la Ekaristi Takatifu limetajwa wapi katika agano la kale?.

Ekaristi Takatifu imeweza kuelezewa na kufananishwa na Mana iliyoshuka kutoka mbinguni kwa wana wa Israeli walipokua jangwani baada ya kumnung'unikia Mwenyezi Mungu kupitia mtumishi wao Musa. Rejea;

(Kut 16:4) “ndipo bwana akamwambia Musa, tazama mimi nitawanyeshea ninyi mvua ya mkate kutoka mbinguni; na hao watu watatoka nje na kuokota kila siku sehemu ya siku; ili nipate kuwajaribu, kwamba watakwenda katika sheria yangu, ama sivyo.”  Tunaona Mungu anawashibisha wana wa Israeli chakula kutoka mbinguni (Mana) ambamo kupitia chakula hicho, jina lake liweze kutukuzwa, Vivyo hivo hata sasa Mwenyezi Mungu anatulisha mwili na damu ya mwanae kupitia Mafumbo ya Ekaristi Takatifu ili kupitia huo naye kukaa kwetu, tupate neema za kuishi kwa kadri ya sheria yake.

Vilevile imeandikwa; (kut 16:16-18) "Neno hili ndilo aliloagiza Bwana, Okoteni ninyi kitu hicho kila mtu kama ulaji wake ulivyo; kichwa pishi, kama hesabu ya watu wenu ilivyo; ndivyo mtakavyotwaa, kila mtu kwa ajili ya hao walioko hemani mwake. Wana wa Israeli wakafanya hivyo, wakaokota wengine zaidi, wengine kupungua. Nao walipoipima kwa pishi, yeye aliyekuwa ameokota kingi hakubakiwa na kitu, na yeye aliyekuwa ameokota kichache hakupungukiwa; wakaokota kila mtu kama ulaji wake ulivyokuwa."  

Hivo kupitia mstari tajwa hapo juu, Kristo anajihirisha katika Ekaristi Takatifu ya agano jipya ambapo kama wakristo wakatoliki, apokeae Ekaristi nusu (kiumbo) na yule aliyepokea mkate mzima wote ni sawa na wanampokea Kristo aliye kamili katika roho zao wala hakuna anayepungukiwa, wala kuzidishiwa.

 

   Fumbo la Ekaristi Takatifu katika Agano jipya.

Fumbo hili la mwili na damu ya Bwana wetu Yesu Kristo, katika agano jipya linadhihirishwa kwanza katika karamu ya Mwisho siku ya Alhamisi kuu Kristo alipoketi na mitume wake kuumega mkate

Turejee; (Lk 22:19-20) “Akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema, [Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Kikombe nacho vivyo hivyo baada ya kula; akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu.].”  

Vilevile katika barua ya Mtume Paulo (1 Kor 11:23-26)  “Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo.”

 

   Je, Ekaristi Takatifu ina nguvu au umuhimu gani kwa mkristo?

(Gal 2:20) “Nimesulibiwa pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu, ambaye alinipenda, akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu”. Basi wakristo wenzangu, tuulapo mwili wa Kristo na kukinywea kikombe chake si sisi tena tunaojiongoza bali ni kristo ndiye aishiye ndani yetu.

Hivo Kristo anatulisha mwili wake katika Ekaristi Takatifu ili kwa imani tubadilishwe kutoka katika madhaifu yetu na kupokea umungu wake na ustahimilivu katika kuyashika maagizo yake na kuiepuka dhambi. Mfano; Ni wazi kwamba, kwa hali ya kawaida na katika madhaifu ya ubinadamu wetu yaweza kuwa ngumu sana kumsamehe jirani yako aliyekukosea. Lakini kwa nguvu ya Kristo yote yawezekana, yaani twaweza kusamehe kwa wepesi na kusahau kwani si sisi tena tunaotenda kazi peke yetu, bali ni Kristo anayeishi ndani yetu ndiye aitendaye kazi yake. Kumbe basi, twaweza kuepuka hatari ya dhambi zote katika yeye atutiaye nguvu, rejea; (Flp 4:13) “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”

 

   Je, twapaswa kupokea Ekaristi Takatifu tukiwa katika hali gani?

Twapaswa kupokea mwili na damu ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwanza tukiwa na neema ya utakaso, yaani tusiwe na dhambi ya Mauti (Dhambi tunazozifanya kwa makusudi, kwa  kujiambua, na kwa hiari, kwani tunaamua kwa akili zetu kuyafanya mapenzi yetu na kuyapuuza mapenzi ya Mwenyezi Mungu, hivo tunajitenga kabisa na  upendo wa Mungu na kukosa ushirika naye.)

Pili, kwa kuungama dhambi nyepesi kila mara tunapoanguka, (kuhusu dhambi kubwa na dhambi nyepesi rejea, 1 Yoh 5:16-17). Tatu tunaaswa kufunga kabla ya adhimisho la Misa Takatifu ili kuandaa roho zetu kumpokea Kristo kwani yeye ndiye uzima wetu na tumaini letu na Nne twapaswa kumtambua, kumwamini na kumkiri Kristo aliye kweli katika maumbo ya mkate na divai kuwa ndiye mwokozi wa maisha yetu na muweza wa yote atupatiaye nguvu ya kuyashinda majaribu yote.

 

   Je, kuna Madhara gani ya kupokea Ekaristi Takatifu, isivyostahili?.

Imeandikwa; (1 Kor 11:27-32) “Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana. Lakini mtu ajihoji mwenyewe, na hivyo aule mkate, na kukinywea kikombe. Maana alaye na kunywa, hula na kunywa hukumu ya nafsi yake, kwa kutokuupambanua ule mwili. Kwa sababu hiyo wako wengi kwenu walio hawawezi na dhaifu, na watu kadha wa kadha wamelala. Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa. Ila tuhukumiwapo, twarudiwa na Bwana, isije ikatupasa adhabu pamoja na dunia.”

Hivyo, wakristo wenzangu, tunapopokea Ekaristi Takatifu isivyotahili (kama vile kuwa na dhambi ya mauti, kutokuwa na uelewa kamili wa kile tunachoenda kukipokea na kupokea kwa mazoea) au katika hali isiyo ya utakatifu, kwanza ni kufuru juu ya Sakramenti, na pili twaupokea mwili na damu yake Bwana wetu Yesu Kristo lakini sio neema zake. Hivo tunakosa neema ya Kristo kujidhihirisha katika maisha yetu na matendo yetu.

Shetani huendelea kufanya kazi katika maisha yetu kama ilivyokuwa awali tukiwa wadhambi na kabla ya kupokea nguvu ya Kristo kupitia Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. tunaona ambavyo Yuda mwana wa Iskariote alivyoshindwa kukiri makosa yake mbele ya Kristo na maamuzi yake ya kumsaliti Kristo kabla ya karamu ya mwisho, naye alipopokea mkate shetani alimwingia na akaendelea kufanya kile alichokipanga bila ya kufaidika chochote kwani alimpokea Kristo lakini sio neema zake kulingana na dhambi alokuwa nayo. Turejee (Yn 13:26-27) “Basi Yesu akajibu, Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa. Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwa mbia, uyatendayo yatende upesi.”

 

Hitimisho.

   Ekaristi Takatifu ni fumbo linalonoa uhusiano wetu na Mwenyezi Mungu, linaimarisha roho zetu na hamu ya kuendelea kumtafuta yeye, hivo kama wakristo wabatizwa na tuliopokea Sakramenti ya Komunyo twapaswa Kupokea Ekaristi Takatifu mara kwa mara katika hali ya utakatifu na tafakari ili zile neema zinazopatikana kupitia kuupokea mwili na damu wa Bwana wetu Yesu Kristo zitusaidie kuyabadili maisha yetu kutoka ukale usiofaa na tuweze kuyaishi mafundisho yake kwa Imani na matendo.

   Tukumbuke kwamba, tunayotenda dhambi tunapoteza uhusiano wetu na Mungu, ambapo bila Baba hakuna Mwana, hivo tunakosa ushirika tena na Kristo kwa kumkaribia shetani na maovu yake, hivo tuzidi kuimarisha uhusiano wetu na Mwenyezi Mungu kwa kufanya Toba kila tunapoanguka, tudumu katika njia njema na tuzidi kujiimarisha kupitia nguvu ya Kristo kupitia fumbo la Ekaristi Takatifu.

   Basi, Tumwombe Mwenyezi Mungu atuongezee imani juu ya Fumbo hili la Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu kristo, Mungu-mtu katika maumbo ya mkate na Divai, na imani hiyo itujapatie nguvu za kuuishi ukristo wetu na mapendo kwa jirani zetu katika mazingira na maisha yetu ya kila siku mwisho tufike kwake juu mbinguni.

Tumsifu Yesu kristo...

 

 

Post a Comment

Previous Post Next Post